| MABAO yaliyofungwa na Hamis Kiiza na Said Bahanuzi yameipa ubingwa wa mara tano Yanga wa Kombe la Kagame.
Kwa ushindi huo Yanga ambao walikuwa mabingwa watetezi wamefanikiwa kutetea ubingwa wao, huo kwa mara nyingine tena.
Mchezo huo ambao ulitawaliwa na vituko vingi kabla ya kuanza nahodha wa Azam, Agrey Morris alikataa kupeana mikono na mwenzake wa Yanga, Nadir Haroub.
Mchezo huo ulianza kwa kasi huku Azam wakionekana kutaka kupata bao la mapema, ambapo iliwachukua dakika mbili kabla ya John Boko kulifikia lango la Yanga lakini alipiga shuti lilotoka nje.
Dakika 12 baadae, Kipre Tchetche kama angekuwa makini angeweza kuipatia Azam bao la kuongoza.
Azam waliendelea kulisakama lango la Yanga ambapo dakika ya 15 walipata kona iliyopigwa na Abubakar Salum na kuungwanishwa na Moris kwa kichwa na mpira kumgonga Ally Mustapha.
Yanga walijibu shambulizi hilo kwa Haruna Niyonzima kuwalamba chenga mabeki wa Yanga na kupiga krosi safi iliyookolewa kiufundi na Deogratius Munishi.
Baada ya kuona mashambulizi yamezidi kocha wa Yanga, Tom Sainttief alimuita Niyonzima na kumweleza kitu ambapo baada ya hapo ‘alijiungashusha’ na kujidai ameaumia huku kocha huyo akitumia muda huo kuwaita wengine na kuwapa maelekezo.
Azam walitawala kabisa mchezo huo kwa dakika 30 za mwanzo huku wenzao wa Yanga wakipoteana kabisa.
Dakika 30 Bahanuzi alifanikiwa kuwalamba chenga mabeki wa Azam ndani ya eneo la hatari lakini alitoa pasi ambayo ilitoka nje.
Rashid Gumbo alipiga shuti kali dakika ya 34 ambalo lilitemwa na Munishi na kumkuta Bahanuzi ambaye alipiga nje.
Uzembe uliofanywa na Agrey Moris kwa kumudishia mpira mfupi Munishi ambao uliwahiwa na Kiiza aliyepiga shuti na kumgonga kipa na kujaa wavuni.
Kipindi cha pili kilianza kwa David Luhende kuwalamba chenga wachezaji wa Azam na kumpa pasi safi Gumbo ambaye alipiga shuti lilodakwa na Munishi.
Yanga ambao walionekana kupata nguvu zaidi kipindi cha pili, waliendelea kulisakama lango la wapinzani wao.
Kama Kiiza na Niyonzima wangekuwa makini wangeweza kuipatia Yanga mabao dakika za 58, 82 na 86.
Mabeki wa Azam watajutia makoa waliyofanya katika mchezo huo ambapo walitegeana kuokoa mpira ambao uliwahiwa na Bahanuzi na kuachia shuti kali lilojaa wavuni na kuipatia Yanga bao la pili.
Kikosi: Ally Mustapha, Nadir Haroub, Stephano Mwasika, Kelvin Yondani, David Luhende, Athuman Iddy, Rashid Gumbo/Juma Seif, Oscar Joshua, Hamis Kiiza, Said Bahanuzi na Haruna Niyonzima.
Azam FC: Deogratiu Munishi, Ibrahim Shikanda, Said Morad, Erasto Nyoni, Aggey Moris, Jabir Aziz/George Odhiambo, Kipre Tchetche/Mrisho Ngasa, Salum Abukar, John Boko, Ibrahim Mwaipopo na Ramadhani Chombo.
Baada ya mchezo huo kocha mkuu wa Azam FC, Stewart Hall, alisema kikosi chake kimecheza vizuri huku akitoa sifa nyingi kwa kiungo wake chipukizi Abubakar Salum.
Alisema kikosi hicho hakitabadilika katika ligi kuu msimu ujao na kuwaongezea mazoezi kwa ajili ya ligi hiyo.
Pia aliongeza kuwa John Boko ameshindwa kufanya vile ambavyo alitegemea baada ya kucheza katika kiwango cha chini.
Alisema kupoteza mchezo huo kumetokana na kutotumia nafasi ambazo walipata huku wapinzani wao wakizitumia.
Kwa upande wake kocha wa Yanga alisema Tom Saintfiet alisema anashukuru ameanza vizuri katika timu hiyo kwa kunyakuwa kombe la kwanza.
Alisema timu ya Azam ni kati ya timu bora ambayo ina viungo wengi wazuri, ambapo kama itatunzwa itakuja kuwa bora zaidi baadae kutokana na kuwa na wachezaji wengi vijana.
Alisema anawashukuru wachezaji wake kwa kufuata maagizo yake japokuwa ailikuwa katika kipindi kifupi toka alipojiunga na timu hiyo.
Wakati huo huo Said Bhanuzibaliyesajiliwa na timu hiyo alitokea Yanga amefanikiwa kuibuka mfungaji bora wa michuano hiyo kwa kufunga mabao sita.
Kutokana na kunyakuwa ubingwa huo Yanga imefanikiwa kupata kitita cha dola 30,000, Azam walioshika nafasi ya pili wamepata dola 20,000 huku Vita ya Kongo DRC iliyoshika ya tatu ikipata dola 10,000.
Wakati huohuo, Mwenyekiti wa Yanga, Yussuf Manji alionekana ntu mwenye furaha kubwa kuliko mwingine yoyote katika matokeo hayo.
Manji ambaye aliapa ataifanyia kweli Azam kabla ya mchezo huo, alionekana mwenye furaha kubwa wakati wote huku akicheza wakati mwingi wa mchezo.
“Achana na Manji, yaani kama kuna kitu kimemfurahisha ni leo,” alisema shabiki mmoja.
Naye mshambuliaji Said Bahanuzi, aliwakosha zaidi mashabiki wa Yanga kutokana na kufunga bao hilo katika dakika za nyongeza. |