|
* Wamchoka Phiri
Na Chausiku Omary
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu Bara, Simba inatarajia kuondoka Keshokutwa kwenda kuweka kambi Visiwani Zanzibar kwa ajili ya maandalizi ya ligi kuu Bara itakayoanza Agosti 21.
Simba imekuwa na mafanikio makubwa katika ligi zake pindi wawekapo kambi kisiwani humo, hivyo kuna matuamaini makubwa kwa timu hiyo kuutetea ubingwa wake.
Mabingwa hao waliochini ya makocha, Suleiman Matola na Amri Said, walianza mazoezi mwanzoni mwa mwezi huu kwa kuanza mazoezi ya gym na kufuatiwa yale ya ufukweni kabla ya kuanza mazoezi ya uwanjani.
Akizungumza na Spoti Starehe jana, Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Godfrey Nyange 'Kaburu' alisema baada ya kukamilisha taratibu zote za kutangaza majini ya wachezaji waliosajili msimu huu wanatarajia kujichimbia visiwani humo ili kuhakikisha timu yao inafanya vizuri katika ligi hiyo
"Tunatarajia kuondoka Jumamosi na kikosi kamili cha wachezaji 26 tuliowatangaza, pamoja na Kocha mkuu Patrick Phiri kama atakuja lakini akishindwa kufanya hivyo tutakuwa na Matola na Amri," alisema Kaburu.
Kaburu alisema wanaamini kuwa watatetea ubingwa wao kutokana na kuwa na kikosi imara walichosajili msimu huu kwa kuzingatia mahitaji ya timu hiyo kwa ajili ya ligi hiyo na michuano ya kimataifa.
Wachezaji wapya waliongezwa katika kikosi hicho ni Mohamed Aziz, Amir Maftah, Abdulhalim Humoud, Shija Mkina, Mganda Patrick Ochang, Mbwana Samatta na Rashid Gumbo, sambamba na mchezaji Kelvin Charles kutoka timu ya U-20.
Wachezaji wengine ni Makipa Juma Kaseja, Ally Mustapha 'Barthez', Salumu Kanoni, Haruna Shamte, Juma Jabu, Kelvin Yondan, Juma Nyosso, Joseph Owino na David Naftari, Mohamed Banka, Jerry Santo, Hillary Echessa, Amri Kiemba, Nico Nyangawa, Uhuru Selemani, Salum Aziz 'Gilla', Emmanuel Okwi, Mussa Hassan 'Mgosi' na Mohamed Kijuso.
Wakati huo huo, Nyange alisema wamempa Phiri nafasi ya mwisho ya kutimiza ahadi yake, kama akishindwa kufanya hivyo wataachana na kocha huyo na kuangalia mambo mengine.
Kaburu alisema Phiri amekuwa akitoa ahadi nyingi lakini ya mwisho ameahidi kuja nchini kesho kwani atakuwa amemaliza matatizo yake huko kwao Zambia, lakini akishindwa hatutaendelea kumfuatilia tena.
Simba wapo katika mazungumzo na Kocha wa Uganda, Sam Timbe ambaye ananafasi kubwa ya kuchukua nafasi ya Phiri na Silleysaid Mziray ambaye atakuwa msaidizi wake. |